|
|
Posted by monfinance on October 20, 2012 in Finance,Taxation and Investment, Tanzania News
Tags: Tanzania business News, Tanzania Revenue Authority., TRA, VAT Returns
MFblog Inaendelea kuleta matukio yanayoendelea Mjini Dodoma katika kipindi hiki cha kikao cha Bunge cha bajeti. “ALL EYES ON DODOMA-BUNGENI”

Mh. Zitto Kabwe
WAZIRI Kivuli wa Fedha Kabwe Zitto amewasilisha bungeni bajeti mbadala ya Kambi ya Upinzani kwa mwaka wa fedha 2012/2013.
Zitto amebainisha kasoro nyingi zilizopo katika bajeti ya Serikali iliyowasilishwa bungeni Alhamisi iliyopita.
Bajeti ya Zitto ilitanguliwa na hotuba ya Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani kuhusu Ofisi ya Rais – Mipango, Christina Mughwai ambaye pia alibainisha alichokiita udhaifu wa Serikali katika kuitekeleza mipango yake ya kiuchumi.
Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni katika hotuba yake alisema mapato ya Serikali yanaweza kuongezwa kwa Sh2.885 trilioni, hivyo kupunguza utegemezi wa mikopo ya kibiashara ambayo imekuwa ikiligharimu taifa kiasi kikubwa cha fedha. Vyanzo vya kodi na kiasi cha fedha kwenye mabano alivyopendekeza ni marekebisho ya kodi za misitu ukiwemo mkaa (Sh130.8 bilioni), kupunguza misamaha ya kodi, kuzuia ukwepaji kodi na udanganyifu wa biashara ya nje (Sh742.74 bilioni), mauzo ya hisa za Serikali (Sh415.55 bilioni), Marekebisho ya kodi Sekta ya Madini na asilimia 25 ya Mauzo ya Madini Nje (Sh578.36 bilioni) na Marekebisho ya Kodi na Usimamizi bora wa Mapato Kampuni za Simu (Sh502.26 bilioni).
Mapendekezo mengine ni Marekebisho ya Kodi ya Tozo ya Kuendeleza Stadi (Sh243.52 bilioni), mapato ya wanyamapori (Sh61.64 bilioni), kuondoa msamaha wa ushuru wa mafuta kwa kampuni za madini (Sh44.9 bilioni), Usimamizi wa mapato ya utalii (Sh51.75 bilioni), Kuimarisha biashara Afrika Mashariki (Sh 114.15 bilioni).
Zitto alisema kama wapinzani wangekuwa madarakani wangekusanya kiasi cha Sh15 bilioni sawa na ile ya Serikali, lakini tofauti ni hatua ya kutenga asilimia 35 ya mapato ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kupunguza utegemezi wa bajeti kutoka asilimia 42.37 za Serikali hadi asilimia 21.3.
Amesema, Serikali haipaswi kuendelea kukopa, kwani taarifa rasmi za kibenki na ukaguzi wa hesabu zinaonyesha kwamba deni hilo linakua kwa kasi tofauti na maelezo ya Serikali kwamba linahimilika.
“Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali inaonyesha kuwa Deni la Taifa linazidi kuongezeka kwa asilimia 38 kutoka Sh10.5 trilioni mwaka 2009/2010 hadi Sh14.4 trilioni 2010/2011. Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha, Deni la Taifa limefikia Sh20.3 trilioni mpaka ilipofika mwezi Machi mwaka 2012,”
alisema Zitto na kuongeza: “Ukisoma taarifa ya Mwezi wa Mei 2012 ya Benki Kuu ya Tanzania, Deni la Taifa sasa limefikia Sh22 trillion. Suala hapa sio ustahmilivu wa Deni kama inavyodai Serikali, bali ni kwamba tunakopa kufanyia nini?”
Alisema hesabu za bajeti ya Serikali ya 2012/13 inayopendekezwa zinaonyesha kwamba Serikali bado ina mpango wa kukopa kwa ajili ya kugharamia matumizi ya kawaida ambayo hayazalishi wala kutozwa kodi. “Hatutaki mikopo kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya posho, kusafiri, magari n.k. Tuchukue mikopo kuwekeza kwenye miradi itakayokuza uchumi na kuzalisha kodi zaidi,” alisema.
Kuhusu mfumuko wa bei, Zitto alikosoa hatua zinazopendekezwa na Serikali kukabiliana nao, kwamba ni zile zilizoshindwa katika mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, mwaka huu. Alisema hatua hizo ambazo ni kutoa vibali kwa wafanyabiashara vya kuagiza mchele na sukari bila kutoza kodi, haziwezi kusaidia kwa kuwa hatua kama hizo zilipochukuliwa awali zilisababisha bei ya bidhaa hizo kuongezeka. “Baada ya hatua hii bei ya sukari ilipanda kutoka Sh1,700 mpaka 2,800 kwenye maeneo mengi nchini… Serikali inachukua hatua zile zile kwa tatizo lile lile ikitegemea matokeo tofauti,” alisema Zitto.
Alirejea pendekezo la mwaka jana kwa Serikali kutoa vivutio kwa wakulima wadogo kuzalisha chakula kwa wingi akisema kuwa hatua hiyo pekee ndiyo itapunguza mfumuko wa bei. “Hakuna mbadala wa kudhibiti mfumuko wa bei zaidi ya kuongeza uzalishaji wa chakula na kuwekeza kwa wananchi wetu.
Serikali inafikiria uzalishaji utaongezeka kwa kusaidia wakulima wakubwa ambao watageuza wananchi wetu kuwa manamba na vibarua ndani ya nchi yao,” alisema na kuongeza: “Tuwekeze kwa watu wetu vijijini ili waongeze uzalishaji na kwa kufanya hivyo mfumuko wa bei ya chakula utakuwa historia. Hakuna mwarobaini wa kupanda kwa bei za vyakula isipokuwa kilimo”.
MF: Well done Zitto; Tunaendelea Kufuatilia yanayoendelea Dodoma kwa Ukaribu.
Posted by monfinance on June 19, 2012 in Tanzania News
Tags: Bajeti ya Tanzania, Bajeti ya Tanzania 2012, Bajeti ya Upinzani, monfinance Blog, Tanzania budget, Tanzania Economy, Tanzania Revenue Authority., Taxation, Zitto Kabwe
Dodoma, Tanzania: SERIKALI imetangaza bajeti ya shilingi trilioni 15 kwa mwaka wa fedha 2012/2013.
Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, pamoja na mambo mengine, bajeti hiyo imelenga kudhibiti mfumuko wa bei kwa kutangaza kutoa vibali vya kuingiza chakula kutoka nje, na kuwabana matajiri kwa kuongeza kodi ya bidhaa zisizokuwa za lazima.
Akisoma bajeti hiyo bungeni mjini Dodoma jana, Dk Mgimwa pia alitangaza kwamba Serikali imepanua wigo wa Kodi ya Mishahara (Paye) na sasa itawagusa wafanyakazi wenye kipato cha kuanzia Sh170,000 badala ya Sh135,000 ya awali.
Amesema, Serikali pia imerejesha mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kwa kutenga Sh7 bilioni kwa ajili ya kuchukua vijana 5,000.
Dk Mgimwa amelieleza Bunge kuwa, Serikali imeongeza kodi za bidhaa mbalimbali, zikiwemo, bia, soda, sigara, juisi zinazoingizwa kutoka nje na kufuta msamaha wa ushuru wa bidhaa kwa magari kwa wote waliokuwa wananufaika na msamaha huo.
Alifafanua kwamba kodi ya vinywaji baridi imepanda kutoka Sh69 kwa lita hadi Sh83 na mvinyo unaotengenezwa kwa zabibu inayozalishwa nchini kwa kiwango kinachozidi asilimia 75, imeshuka kutoka Sh425 kwa lita hadi 145 kwa lita.
Wabunge wameelezwa kuwa, kodi ya mvinyo unaotengenezwa kwa zabibu inayozalishwa nje ya nchi kwa kiwango kinachozidi asilimia 25, imepanda kutoka Sh1,345 kwa lita hadi 1,614 kwa lita.
Dk Mgimwa amesema, kodi ya vinywaji vikali imepanda kutoka Sh1,993 kwa lita hadi Sh2,392 kwa lita, bia inayotengenezwa nchini kwa nafaka na ambayo haijaoteshwa, kodi yake imepanda kutoka Sh248 kwa lita hadi Sh310 kwa lita. Bia nyingine zote kodi imepanda kutoka Sh420 hadi Sh525 kwa lita.
Kuhusu ushuru wa bidhaa za sigara, Dk Mgimwa alisema, sigara zote zisizo na kichungi na zinazotengenezwa kwa tumbaku inayozalishwa nchini, kiwango cha angalau asilimia 75, kodi imepanda kutoka Sh6,820 hadi Sh 8,210 kwa sigara 1,000.
Alisema Sigara zenye kichungi na zinazotengenezwa kwa tumbaku inayopatikana nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75, kodi imepanda kutoka Sh16,114 hadi Sh19,410 na sigara nyingine zenye sifa tofauti na makundi hayo, kodi imepanda kutoka Sh29,264 hadi Sh35,117 kwa sigara 1,000.
Alisema tumbaku ambayo ipo tayari kutengenezwa sigara (cut filler) kodi yake imepanda kutoka Sh14,780 hadi Sh17,736 kwa bunda la sigara 1,000 wakati ushuru wa cigars unabaki kuwa asilimia 30.
Katika bajeti hiyo, Waziri Dk Mgimwa alisema muda wa maongezi (airtime) kwenye simu za mkononi umeongezeka kutoka asilimia 10 hadi 12.
Alisema lengo la hatua hiyo ni kuoanisha ushuru wa bidhaa unaotozwa na huduma hiyo katika nchi za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC), kwa kipindi hiki ambacho nchi zipo katika Soko la Pamoja.
Alisema hatua hizo za ongezeko la ushuru wa bidhaa kwa pamoja, zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha Sh144,054.9 milioni.
Waziri huyo alipendekeza kufanyika marekebisho kwenye sheria husika za kodi ya matangazo ya Serikali yanayotoa msamaha wa kodi kwenye magari kwa walengwa mbalimbali ili kuweka ukomo wa umri wa miaka minane kwa magari hayo badala ya miaka 10.
Alisema magari yenye umri wa zaidi ya miaka minane yatatozwa ushuru wa bidhaa wa asilimia 20. Lengo la hatua hiyo ni kupunguza wimbi la uingizaji magari chakavu na kulinda mazingira.
Alitangaza pia marekebisho katika ushuru wa forodha, ikiwemo kufuta msamaha wa ushuru wa forodha katika vitu mbalimbali vikiwemo magari yenye ujazo wa CC 3000 huku pia ushuru wa forodha ukifutwa katika bidhaa nyingine nyingi muhimu.
Alisema katika kuhamasisha na kuchochea ukuaji wa sekta ya ufugaji wa nyuki, vifaa vinavyotumika katika ufugaji na kurina asali vimepewa msamaha wa ushuru wa forodha vinavyoingizwa kutoka nje ya nchi na wafugaji wa nyuki.
Alisema msamaha wa ushuru wa forodha kwenye migahawa ya majeshi ya ulinzi utaendelea kutolewa kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Alisema kumefanyika marekebisho katika Sheria ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ya mwaka 2004 ili kutoa msamaha wa ushuru wa forodha kwa wazalishaji wa vyakula vinavyotengenezwa mahsusi kwa lishe ya watoto wenye utapiamlo na watu wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi.
Alisema kuwa katika Bajeti hiyo, pia wametoa msamaha wa ushuru wa forodha kwenye malighafi zinazotumika katika kutengeneza vifaa vya kufanyia uchunguzi wa magonjwa (medical diognastic kits) kwa kuwa vifaa hivyo hutozwa asilimia sifuri vinapoagizwa kutoka nje ya nchi.
Katika marekebisho hayo, utatolewa msamaha kwenye mitambo (machinery) na vipuri vyake vinavyotumika kwenye uchimbaji wa madini lakini hautahusisha vipuri vya magari vitakavyoagizwa na makampuni yanayojihusisha na uchimbaji wa madini.
Katika bajeti hiyo, pia umetolewa msamaha wa ushuru wa forodha kwenye vyuma vinavyowekwa kwenye kingo za barabara na lengo lake ni kutoa unafuu katika ujenzi wa miundombinu ya barabara.
Alisema ushuru wa forodha umepunguzwa kwa ving’amuzi kutoka asilimia 25 hadi asilimia sifuri ili kuwezesha mabadiliko katika teknolojia ya analogia na kwenda katika teknologia ya digitali.
Alisema katika Bajeti hiyo, pia ushuru wa ngano umeondolewa kuwa asilimia 0 badala ya asilimia 35.
Alisema Serikali pia imesamehe VAT katika mashine za kutolea stakabadhi (electronic fiscal devices), ili kupunguza bei yake na kuwezesha wafanyabiashara wengi kuwa nazo, kuhamasisha matumizi yake na hivyo, kuongeza mapato ya Serikali.
Katika eneo hilo, Serikali imeondoa VAT kwa vifaa mbalimbali vya kuhifadhia, kusafirisha na kusambaza gesi asilia ili kuongeza matumizi ya nishati hiyo katika sekta mbalimbali za kiuchumi, kwenye magari, majumbani na viwandani.
Wafanyabiashara ambao mapato yao hayazidi Sh3,000,000 hawatalipa kodi kuanzia Julai Mosi, mwaka huu. Dk Mgimwa alisema mpango huo umefanywa kulinda mapato ya Serikali.
Kabla ya msamaha huo, wafanyabiashara hao ambao mapato yao hayazidi Sh3,000,000 walikuwa wanalipa Sh35,000.
Marekebisho mengine ya kodi ya mapato ni kuwa wenye mapato kati ya Sh3 milioni –Sh7.5 milioni watalipa Sh100,000 badala ya Sh95,000.
Waziri Mgimwa alisema Bajeti hiyo imejielekeza katika Kukuza Pato la Taifa kwa asilimia 6.8 mwaka 2012 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 6.4 mwaka 2011.
Malengo mengine ni kuimarisha miundombinu ya uchumi, ikijumuisha umeme, barabara, reli na bandari, kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha na kuongezeka kwa mapato ya ndani yatakayofikia uwiano na Pato la Taifa wa asilimia 18 kwa mwaka 2012/13 kulinganisha na mwelekeo wa asilimia 16.9 mwaka 2011/12.
Dk Mgimwa alitaja malengo mengine kuwa ni pamoja na kuendelea kudhibiti mfumuko wa bei ili urudi kwenye viwango vya tarakimu moja na kuwa na kiwango tengemavu cha ubadilishaji wa fedha kitakachotokana na mwenendo wa soko la fedha.
Malengo mengine ni kukuza mikopo kwa sekta binafsi kwa kiwango cha asilimia 20 ya Pato la Taifa ifikapo mwishoni mwa Juni 2013, sambamba na jitihada za kudhibiti mfumuko wa bei, kuboresha mazingira ya wafanyabiashara wadogo na wa kati, kulinda na kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika sekta za huduma za jamii, kuimarisha utawala bora na uwajibikaji na kujenga uwezo wa nchi kukabiliana na misukosuko ya kiuchumi na kifedha pamoja na kushiriki kwa ufanisi katika ushirikiano kikanda na kimataifa.
Kuhusu matumizi ya maendeleo, Waziri Mgimwa alisema itazingatia vipaumbele vya miundombinu ya umeme – mkazo ukiwa upatikanaji wake kwa kuongeza uzalishaji, usafirishaji na usambazaji na jumla Sh498.9 bilioni zimetengwa.
Posted by monfinance on June 15, 2012 in Business News, Tanzania News
Tags: Bajeti ya Tanzania 2012, Budgeting, Dar es salaam stock Exchange, Dr.William Mgimwa, General Knowledge, monfinance, Tanzania budget, Tanzania Economy, Tanzania Revenue Authority., Taxation
|
Posted by monfinance on March 13, 2012 in Finance,Taxation and Investment, Tanzania News
Tags: Electronic Cargo Tracking System, General Knowledge, Tanzania Revenue Authority., TRA
"Knowledge is of two kinds. We know a subject ourselves, or we know where we can find information on it” said Samuel Johnson. Well, my name is Monica Joseph, a Tanzanian woman with an all-encompassing experience in all aspects of Taxation, accounting, auditing and financial management. A MSc. Finance degree holder from the University of Strathclyde, and, of course a Social media aficionado, I look forward to the happiest and knowledgeable blogging safari ever, with stops at all issues as mentioned above. JOIN ME & LETS DO IT...
Blog at WordPress.com. Theme: Customized Choco by .css{mayo}.