KAMPUNI ya Ndege ya Tanzania (ATCL) imerejesha safari ya kutoka Dar es Salaam kwenda Hahaya katika visiwa vya Comoro, ikitekeleza mpango wa miaka mitano wa kuongeza idadi ya ndege na safari zake.

Akizungumza baada ya kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Prince Said Ibrahim mjini Hahaya jana, Kaimu Mkurugenzi wa Biashara wa ATCL, Mwanamvua Ngocho alisema, kampuni hiyo itakuwa ikifanya safari zake mara nne kwa wiki katika njia hiyo. ATCL ilifuta safari zake za Dar es Salaam – Hahaya mwaka 2008.
“Tumezindua upya safari yetu ya Dar es Salaam – Hahaya (Comoro) ikiwa ni safari yetu ya kwanza ya kimataifa tangu tuliporejesha utoaji wa huduma miezi miwili iliyopita. Tumeamua kuizindua upya safari hii ili kuitumia vilivyo ndege yetu ya Boeing 700-500 ambayo ilikuwa haina kazi baada ya kumaliza safari ya Dar- es Salaam-Mwanza-Kilimanjaro asubuhi,” alisema Ngocho na kuongeza:
“Tumeamua kuchagua njia hii kutokana na umuhimu wake kiuchumi nchini. Tuna imani kuwa jitihada zetu zitasaidia kuongeza mahusiano mazuri baina ya nchi hizi mbili na vilevile kutoa nafasi kwa abiria kutoka Comoro kusafiri sehemu mbalimbali kupitia Dar es Salaam.”
Alisema, kampuni hiyo bado ina mpango wa kujikita katika kuongeza safari za ndani na nje ya nchi, akizitaja safari hizo kuwa ni Dar es Salaam – Lusaka (Zambia), Dar es Salaam – Johannesburg (Afrika Kusini) na kusisitiza mipango hiyo itakamilika endapo watapata ndege nyingine katika muda mfupi ujao.
“Tayari tuko katika mazungumzo ya kupata ndege nyingine ambayo itatusaidia kujikita katika safari za kimataifa. Katika mpango huo, tutashirikiana kibiashara na baadhi ya kampuni za ndege ili kuweza kulifanikisha hili,” alisema Kaimu Mkurugenzi huyo.
“Bidhaa nyingi zitumikazo nchini Comoro zinatokea Tanzania. Wananchi wanatakiwa kuitumia fursa hii ipasavyo kutokana na ukweli kwamba ATCL itatoa huduma ya usafirishaji kwa bei nafuu,” alisema.
