KAMPUNI ya simu za mkononi (Tigo), imezindua huduma ya Tigo Jamaa yenye lengo la kusaidia kuwaunganishia wateja wao na huduma za intaneti kwenye simu zao.
Meneja Mradi wa Intaneti wa Tigo, Titus Kafuma amewaeleza waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kuwa, watu wengi wana simu zenye huduma ya intaneti, lakini hawajui jinsi ya kujiunga na kuzitumia.
Kafuma amesema, wametayarisha timu ya Tigo Jamaa itakayosaidia wateja wao kuunganisha simu zao na intaneti kwa haraka na kuwaelekeza matumizi yake bila malipo yoyote.
Kwa mujibu wa Kafuma, wateja wao watafundishwa kusoma barua pepe, kutumia mtandao wa Facebook, kusoma habari za michezo, fasheni, habari kupitia tovuti mbalimbali, twitter ili kuwapa fursa ya kufurahia kifurushi cha intaneti.
Huduma hiyo itaanza kutolewa kesho Dar es Salaam na kisha itaendelea kutolewa mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Morogoro, Dodoma, Mwanza na Tanga kwa watu wenye simu zenye uwezo wa kuunganishwa.
Kwa upande wake, Ofisa Uhusiano wa Kampuni hiyo, Alice Maro alisema, “tunataka kuongeza uwezo wa wateja wetu katika matumizi ya intaneti na tunawakaribisha kwa wingi ili wanufaike na huduma hii.”