TANZANIA ina gesi yenye thamani ya Sh trilioni 626.71, fedha ambazo zinaweza kutosheleza bajeti ya nchi kwa zaidi ya miaka 40 ijayo.
Fedha hizo zinatosha kwa bajeti kuu kwa miaka hiyo iwapo itakuwa Sh trilioni 15 kama ilivyo bajeti ya mwaka huu wa fedha unaoanza Julai mwaka huu.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akijibu hoja mbalimbali za wabunge kuhusiana na Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu , alisema Tanzania ina gesi za ujazo wa futi trilioni 26.99 hadi sasa ambayo ni sawa na mapipa ya mafuta bilioni 4.86.
“Mapipa hayo nikipiga hesabu kwa pipa moja dola za Kimarekani 86 ni sawa na thamani ya gesi yetu dola za kimarekani bilioni 400.81 ambazo ni sawa na Sh trilioni 626.71 ikiwa dola moja ya Kimarekani Sh 1,500 ilivyo sasa,” alisema Waziri huyo.
Alisema hadi sasa zimeshatumika dola za Kimarekani milioni 840 kwa ajili ya utafiti, majaribio na malipo ya mshauri kuhusiana na uchimbaji wa gesi.
Muhongo alisema kabla ya mwisho wa mwaka huu Serikali italeta bungeni muswada wa sheria ya gesi na pia sera ya gesi kwa sasa inatengenezwa ambapo alisisitiza kuwa wataenda katika mikoa ya Lindi na Mtwara kukusanya maoni ya wananchi.
Akizungumzia kuhusu mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, alisema Serikali imetenga Sh bilioni 40 kwa ajili ya kuuchukua mgodi huo moja kwa moja.
Hadi Novemba mwaka jana mkopo wa mgodi huo ulikuwa Sh bilioni 32.24. Mgodi huo una makaa ya mawe tani milioni 50.94.